Saturday, October 18, 2008

JK katika hatua za mwisho za ziara yake Mbeya
Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya CRDB Dr. Charles Kimei akiwatambulisha kwa JK baadhi ya wafanyakazi wa benki hiyo baada ya Rais kikwete kufungua tawi la benki hiyo katika mji wa Mbozi
JK akifunua jiwe la msingi wakati alipofungua rasmi jengo jipya la Halmashauri ya wilaya ya Mbarali jana.Rais Kikwete alikuwa katika ziara ya kikazi ya siku kumi ambapo alikagua na kuzindua miradi mbalimbali ya maendeleo mkoani humo.
JK akikagua Mfereji wa Umwagiliaji mashamba ya mpunga ya wakulima wadogo wadogo huko Uturo,wilayani Mbarali jana.

JK akifunua jiwe la msingi wakati alipofungua rasmi jengo jipya la Halmashauri ya wilaya ya Mbarali jana.
Baadhi ya watoto wa shule wakimshangilia JK na Mama Salma Kikwete muda mfupi baada ya kuwasili katika uwanja wa kanisa katoliki la Mtakatifu Boniface ambapo JK aliwahutubia wananchi wa kata ya Madibira katika mkutano mkubwa wa hadhara

JK akiwahutubia mamia ya wakazi wa mji mdogo wa Chunya wakati alipokuwa katika ziara ya wilaya ya Chunya mkoani Mbeya.
Mwenyekiti wa umoja wa wachimba madini wadogowadogo wilayani Chunya Bwana George Mwaikela akiteta jambo na JK muda mfupi baada ya JK kuwahutubia wananchi wa wilaya ya Chunya katika eneo la Mkwajuni wilayani humo jana.
JK akitaniana na msanii chipukizi aliyejitambulisha kwa jina la Mahuga Bulyaga baada ya Rais Kikwete kuhutbia mkutano wa hadhara kastika eneo la Mkwajuni wilayani Chunya.
JK akimpa msaada wa pesa kijana mlemavu ambaye hana mikono aliyekuwa miongoni mwa wakazi wa mji wa Mbozi walio hudhuria sherehe za ufunguzi wa tawi la benki ya CRDB Tawi la Mbozi. Mama Salma Kikwete amesimama pembeni shoto
JK akisalimiana na baadhi ya madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Mbarali muda mfupi kabla ya kufugnua jemngo jipya la halmashauri hiyo jana. Picha zote na mdau Freddy Maro wa Ikulu


Rais Kikwete ashtushwa na mauaji Mbeya

Na Mwandishi Maalum, Mbarali, Mbeya

Mauaji mengi katika wilaya ya Mbarali, Mkoani Mbeya yanasababishwa na imani za kishirikina na ulevi wa kupindukia, Rais Jakaya Mrisho Kikwete ameambiwa katika siku yake ya nane (jana Ijumaa) ya ziara yake ya siku 10 mkoani humo.


Mkuu wa Wilaya hiyo, Hawa Ngulume amemwambia Rais Kikwete kuwa katika mwaka mmoja uliopita kiasi cha wananchi 102 wa wilaya hiyo wameuawa kwa sababu mbali mbali, idadi iliyomshtua Rais Kikwete.


Mkuu huyo wa wilaya alikuwa akiwasilisha taarifa ya Serikali ya wilaya yake kwa Rais Kikwete kwenye eneo la Uturo, mwanzoni tu mwa ziara ya siku moja katika wilaya hiyo.


"Idadi hii ya mauaji iko juu sana kwa wilaya moja katika mwaka mmoja. Kuna nini? Nielezeni nini sababu ya mauaji kuwa mengi kiasi hiki katika wilaya yenu," Rais amemtaka mkuu huyo wa wilaya kueleza.


Akisaidiwa na uongozi wa jeshi la polisi wilayani humo, Ngulume amesema kuwa sababu kubwa za kiwango cha mauaji kuwa juu sana katika wilaya hiyo ni imani za kishirikina, ulevi wa kupindukia na wizi wa mifugo.


"Kuna unywaji mwingi sana wa pombe katika wilaya yangu, Mheshimiwa Rais," amesema Ngulume na kuongeza kuwa ushirikina umekuwa unasababisha watu kuuawa na kukatwa viungo vyao vya mwili kwa imani kuwa vinaweza kutumika katika kuwaletea watu utajiri.


Na kama ambavyo imekuwa katika wilaya karibu zote za Mkoa wa Mbeya wakati wa ziara hiyo, Rais Kikwete ameelezwa idadi kubwa ya watoto wa shule na wanafunzi wa kike walioachishwa masomo kwa kupewa mimba.


Kwa mwaka mmoja uliopita, kiasi cha watoto 38 wa shule za msingi na wanafunzi 34 wa shule za sekondari katika wilaya hiyo wamepewa mimba. Kesi 72 zinazohusiana na mimba hizo zimeripotiwa polisi.


"Hivi nyie madiwani mnakaa chini na kulijadili suala hilo. Hili ni jambo linakera mno. This is very serious. Hili ni tatizo la jamii na wala siyo la polisi kama mnavyotaka kunieleza," amesema Rais.


"Msipochukua hatua za kuwaadhibu watu wanaozalisha watoto wa shule, watu hawa watazoea. Watageuza shule kama sehemu zao za kuwindia. Hali hii hii nimeikuta kila wilaya katika mkoa huu," amesema Rais Kikwete akiwa anaonyesha wazi kuchukizwa na hali hiyo ya mimba za watoto wa shule.


Baada ya kupokea taarifa hiyo, Rais Kikwete alizindua mradi wa umwagiliaji katika eneo hilo hilo la Uturo, na akaelekea katika makao makuu ya wilaya katika eneo la Lujewa, ambako amefungua Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali na kuwasalimia wananchi.


Akiwa njiani kwenda Madibira ambako alipokelewa na umati wa mamia kwa mamia ya wananchi na kuhutubia mkutano mkubwa wa hadhara, Rais Kikwete amesimama kuangalia hali ilivyo katika Bonde la Ihefu, baada ya Serikali kuwa imeamuru kuondolewa kwa mifugo yote katika bonde hilo.

Serikali iliamuru mifugo yote kuondolewa katika bonde hilo mwanzoni tu mwa Utawala wa Rais Kikwete.


Hatua hiyo ilichukuliwa katika jitihada za kulinda mazingira kutokana na uharibifu wa mazingira kuathiri kwa kiasi kikubwa kina cha maji katika kituo cha kuzalisha umeme cha Mtera, na Mto wa Ruaha. Hali sasa imeanza kubadilika na kuwa nzuri zaidi.


Kwenye mkutano wa hadhara katika Paroko kongwe la Kanisa Katoliki ya Madibira, Rais Kikwete amewasimamisha mmoja mmoja maofisa na watumishi wa Serikali wanaohusika na huduma za afya, maji, umeme kujibu kero za wananchi kuhusu huduma hizo.


Rais pia amekagua mradi mkubwa wa umwagiliaji wa Madibira ambao umegawiwa katika mashamba madogo madogo ya wananchi binafsi.
Mradi huo ni tofauti na miradi ya umwagiliaji ya Kapunga na Mbarali katika mkoa huo huo wa Mbeya ambayo inaendeshwa na wakulima wakubwa.




No comments: