Sunday, August 31, 2008

Watoto Watatu Wafa Maji Jijini
Dar Es Salaam....
Na Maggid Mjengwa.
Alfajiri ya leo nilikutana na hali hii ya huzuni kubwa kwenye ufukwe wa Oysterbay. Pichani ni Mama wa Marehemu Mama Zainab Mzee( mwenye gauni la bluu)akiwa na majirani zake wa anakoishi Mwananyamala'B'.Kilichotokea;watoto watatu waitwao Mgeni(13)Edgar(15 )na Ibrahim( 16)walikwenda kuogelea baharini jana alasiri.
Hawakurudi nyumbani. Bahati nzuri mtoto mmoja aliweza kwenda kwa wazazi na kuripoti kuwa wenzake wamenasa baharini.Leo alfajiri ndipo miili ya Edgar na Mgeni ilipoonekana kando ya bahari.Mwalimu wa karate Abbas Bwaksi ndiye aliyenitangulia kufika eneo la tukio saa kumi na mbili asubuhi.Nilifika mahali hapo saa kumi na mbili na nusu.Kabla sijaingia kwenye mazoezi ya mchangani nilishangaa kumwona

Mwalimu Bwacksi akiwa amesimama katika hali ya huzuni.Mbele niliwaona akina mama wakiwa wamekaa mbele ya mwili wa marehemu Mgeni.Inauma sana moyoni kumwona mama mzazi akiwa amekaa kando ya mwili wa mtoto wake aliyelala akiwa amekufa.Hakika,hakukuwa na mazoezi tena bali shughuli ya kujipanga kwa ajili ya kumtafuta mtoto Ibrahim ambaye hadi naondoka mahali hapo saa mbili asubuhi alikuwa ameonekana alipo majini,lakini kutokana na mawimbi na kina cha maji,waokoaji wa kujitolea watano walikuwa katika hekaheka za kujaribu kuutoa mwili wa marehemu kutoka majini.Mtandao unanipa tabu kidogo,lakini nikipata nafasi nitajitahidi kutuma picha zaidi za tukio hilo mchana au jioni ya leo. Kwa niaba yenu nyote nawapa pole wafiwa.

No comments: