Tuesday, August 26, 2008

Taarifa ya Utekelezaji wa Mapendekezo
ya Mkataba wa Richmond Kusoma
Bungeni Alhamisi..

SPIKA wa Bunge Samuel Sitta amesema kwamba Alhamisi wiki hii Waziri Mkuu Mizengo Pinda anatarajiwa kutoa taarifa kuhusu maazimio 23 yaliyopendekezwa na kamati iliyoundwa kwa ajili ya kupitia mkataba wa Richmond.
Waziri Mkuu anatarajia kuwasilisha Bungeni taarifa ya utekelezaji wa mapendekezo ya Kamati ya Bunge.Waziri Mkuu atatuambia Serikali imefikia wapi katika kutekeleza mapendekezo yafuatayo ya Kamati ya Bunge:

1. Sheria ya Ununuzi wa Umma ya Mwaka 2004(Public Procurement Act,2004)ipitiwe upya ili kuiboresha kwa kuipa Mamlaka nguvu zaidi za udhibiti na uwezo wa kuchukua hatua pale Sheria na Kanuni zinapokiukwa,badala ya kutoa ushauri tu kama ilivyo sasa.

2. Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma isiwajibike Wizara ya Fedha ambayo nayo ni taasisi ya ununuzi (procurement entity)badala yake iwe chombo huru kinachowajibika Ofisi ya Rais na taarifa zake kuwasilishwa Bungeni.

3.Mikataba kati ya TANESCO na Richmond Development Company LLC na sasa Dowans Holdings S.A,kama ilivyo mikataba kati ya TANESCO na IPTL,SONGAS,AGGREKO na Alstom Power Rentals ipitiwe upya.

4. Mkataba kati ya TANESCO na Richmond Development Company LLC ulikuwa wa uzalishaji umeme wa dharura kipindi ambacho nchi ilikuwa katika hali ngumu ya ukame uliokausha mabwawa yote ya kuzalishia umeme.Kamati Teule inaitaka Serikali kutathmini upya uhalali wa kuwepo na kuendelea kuwepo na mkataba.

5. Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye katika majadiliano yake na Kamati Teule alionyesha kutokuelewa kabisa kilichokuwa kinatendeka na wasaidizi wake,na mwakilishi wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali Wakili wa Serikali Donald Chidowu,ambaye ushiriki wake katika GNT haukuwa na tija yeyote,wawajibishwe na Mamlaka ya juu ya nchi kwa kuchangia kuiingiza nchi katika mkataba wa aibu.

6. Katika mikataba yote na makampuni ya nje Serikali ihakikishe kuwa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni(BRELA)inatumika kikamilifu katika kupata taarifa kamili za kampuni hizo, kama vile wanahisa,mitaji na anwani. Aidha,Ofisi zetu za Ubalozi zilizo sehemu mbalimbali duniani zihusishwe katika majadiliano na makampuni yanayotoka nje ya nchi kwa lengo la kupata taarifa zao za msingi na kuboresha nguvu ya hoja ya Serikali.

7. Wajumbe wote wa GNT ambao ni maafisa waandamizi wa Serikali waliongeza muda wa kuzalisha umeme wa dharura toka miezi 12 hadi miaka miwili wawajibishwe mara moja kwa kushindwa kutumia elimu na ujuzi wao kulinda maslahi ya Taifa.

8. Kamati Teule inapendekeza kwamba Waziri wa Nishati na Madini Mhe.Nazir Karamagi, Mb aliyeshabikia sana uhaulishaji huo,awajibishwe.

9. Kamati teule inapendekeza mabadiliko ya haraka ya uongozi wa TAKUKUR.
Kamati Teule inapendekeza kwamba Waziri wa Nishati na Madini wa wakati huo Mhe.Dk. Ibrahim Msabaha (Mb),Katibu Mkuu Ndugu Arthur Mwakapugi wachukuliwe hatua kali za kinidhamu kwa kuliingiza Taifa kwa makusudi kwenye mkataba na kampuni ya mfukoni ambao umesababisha hasara kubwa kwa nchi.
10. Aidha Kamishna wa Nishati Ndugu Bashir Mrindoko naye achukuliwe hatua za kinidhamu kwa kushindwa kumshauri Katibu Mkuu mpya wa Wizara kuhusu udhaifu wa Richmond Development Company LLC.

No comments: