Monday, January 17, 2011

migomo ya wanafunzi wa elimu ya juu yazidi kupamba moto nchini


Mkuu wa Chuo Kikuu kishiriki Cha Ualimu cha Mkwawa (MUCE),Prof. Philimon Mushi akizungunza na vyombo vya habari mara baada ya kutokea kwa mgomo wa wanafunzi wa chuo hicho leo.
Wanafunzi wa Chuo Kikuu kishiriki Cha Ualimu cha Mkwawa (MUCE) Iringa wakiwa katika mgomo wao leo.


Na Francis Godwin wa Globu ya jamii - Iringa
SAKATA la migomo ya wanafunzi wa vyuo vikuu nchini linaendelea kutikisa nchi baada ya wanafunzi wa mwaka wa kwanza katika Chuo Kikuu kishiriki Cha Ualimu cha Mkwawa (MUCE) mkoani Iringa kufanya mgomo wa kuingia madarasani wakiwashinikiza viongozi wa DARUSO kujiuzulu huku wakiituhumu bodi ya Mikopo kwa kuchelewa kuwapa mikopo yao kwa ajili ya chakula na malazi.

Hata hivyo mgomo huo umepelekea kukamatwa na kuwekwa kizuizini kwa muda mwandishi wa habari wa Globu ya Jamii ambaye pia anawakilisha gazeti la Tanzania Daima na redio ya Over Comers Fm mkoani Iringa kwa madai ya kufika chuoni hapo kuzungumza na wanafunzi bila kuitwa na viongozi wa chuo hicho.

Wakizungumza mbele ya waandishi wa habari waanafunzi hao hao walidai kuwa sababu ya wao kugoma kuendelea na vipindi ni kutokana na fedha hizo za mikopo kwa kila mmoja fedha ambazo zilitakiwa kutolewa januari 14, mwaka huu kuendelea kucheleweshwa hadi sasa na kupelekea baadhi yao kulala bila kula chochote kwa zaidi ya siku moja huku baadhi yao wakishindia maji na vyakula vya kuomba omba mitaani kwa wenyeji.

Pamoja na mgomo huo ambao wanafunzi walidai utamalizaka pale tu bodi ya mikopo itakapotimiza wajibu wake bado wanafunzi hao walieleza kulilalamikia jeshi la polisi mkoa wa Iringa kwa askari wake kutumia risasi za moto juzi usiku wakati wa kuwatawanya wanafunzi hao na mmoja kati ya wanafunzi kunusurika kuuwawa kwa risasi .

Wanafunzi hao walisema kuwa kutokana na kukosa fedha hizo kuanzania mwezi Januari 14 wamekuwa wakiishi kwa shida kutokana na kukosa pesa ya mahitaji muhimu ikiwamo chakula, na kudai kuwa kiasi hicho cha Sh 5,000 wanachopewa kila siku kuwa hakikidhi mahitaji yao.

Waliyataja madai mengine dhidi ya uongozi wa chuo na serikali kwamba ni kucheleweshewa vitambulisho vya bima ya afya ambayo kila mwanafunzi uilipia Sh 50,000, kitabu cha muongozo wa masomo na mgao wa umeme.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Phillemon Mush, alikanusha madai hayo japo alidai kuwa ni kweli wanafunzi wanne walikamatwa na kwa mahojiano kuhusiana na mgomo huo na hatimaye kuachiwa japo hakukuwa na vurugu zozote za kuita polisi kutumia nguvu hata kutumia risasi za moto.

Aidha mkuu wa Chuo hicho, Profesa Mushi alisema uongozi wa chuo umefanya mawasiliano na Bodi ya Mikopo, ambayo imethibitisha kwamba fedha za wanafunzi hao zilianza kuwekwa kwenye akaunti zao tangu Ijumaa.

Alisema wana uhakika mpaka kesho Jumanne taratibu za kibenki zitakuwa zimekamilika na wanafunzi hao watakuwa wamepata fedha zao.

Kuhusu kitabu cha muongozo wa masomo na umeme, Profesa Mushi alisema kinaandaliwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kitakapokuwa tayari kitagawanywa kwa wanafunzi hao

Kuhusu tatizo la umeme chuoni hapo alisema kuwa imekuwa ikisababishwa na mgao wa umeme ambao unaendeshwa nchini nzima na kuwa pale mgao wa umeme unapokuwepo eneo hilo umeme wa jenereta umekuwa ukitumika kusambaza umeme katika vyumba vyote vya kusomea, bwalo la chakula na maktaba ili kuwawezesha wanafunzi kusoma vizuri .


Kuhusu mwandishi aliyekamatwa na kuzuiwa kuendelea kutimiza wajibu wake wa kuchukua habari kwa wanafunzi hao mkuu huyo Prof.Mushi alimwomba radhi mwandishi huyo na waandishi wengine kwa kunyanyashwa na watu wa usalama chuoni hapo na kuwa wanahabari wanawajibu wa kuwasikiliza wanafunzi hao kama sehemu ya kazi yao .

Mwandishi huyu aliwekwa kizuizini katika ofisi za usalama chuoni hapo kwa zaidi ya dakika 15 akihojiwa na kutakiwa kueleza mamlaka ya kufika chuoni hapo ameyapata wapi bila wao kumruhusu kuongea na wanafunzi hao.

Kutokana na tukio hilo waandishi wa habari mkoa wa Iringa kupitia klabu yao ya waandishi wa habari mkoa wa Iringa (IPC) wameeleza kusikitishwa na uamuzi wa wanausalama hao wa chuo kumzuia mwandishi na kumweka kumhoji sababu za kuwasikiliza wanafunzi hao na kuwa kufanya hivyo ni kuzuia uhuru wa vyombo vya habari kutoa habari na uhuru wa wananchi kupata habari za uhakika zaidi.

Katibu wa IPC Frannk Leonard alisema kuwa pamoja na uongozi wa chuo kuomba radhi kwa kitendo hicho ila bado jamii inapaswa kutambua kuwa vyombo vya habari zinawajibu wa kuhabarisha na kwenda moja kwa moja katika maeneo ya matukio na kupata habari kamili kwa kuzungumza na pande zote badala ya kukaa ofisini kupata habari za upande mmoja.

Kamanda wa polisi wa mkoa wa Iringa Evarist Mangalla amethibitisha kuwepo kwa mgomo huo wa wanafunzi chuo cha Mkwawa japo amekanusha madai ya wanafunzi juu ya polisi kutumia risasi za moto kuwatawanya na kuwa hakuna askari polisi aliyekwenda katika mgomo huo Mkwawa na kuwa jeshi la polisi si walinzi wa chuo hicho .
Hadi sasa bado wanafunzi hao wanaendelea na mgomo japo jitihada za mazungumzo zinafanywa na viongozi wa chuo hicho.

No comments: