Tuesday, December 28, 2010

MSAADA TUTANI


Naomba utusaidie kuweka picha hizi na ujumbe huu
kwenye Globu ya Jamii. Tunajua zitawafikia wahusika.

Yaani ni aibu kubwa wakazi wa Sinza “ A”, tumeachiwa matakata nyumbani kwetu kwa zaidi ya mwezi mmoja na siku kadhaa sasa. Juzi tu kabla ya krismas wakusanyaji ushuru wa matakata walipita lakini wananchi wamechukia sana sijui kama kuna hata mmoja alijitokeza kulipa.

Mapanya yaliyokufa mawiki kadhaa yaliyopita harufu zilizoko ndani majumbani kwetu inatisha. Krismas tumebakia na mitakataka ndani. Wengine wamezidiwa ndani ya magetini yao na wameweka nje ya geti zao na ni uchafu wa kutisha.

Hii picha imechukuliwa mtaa mmoja tu maeneo ya karibu na blue-bird guest house kuelekea karibu na hospitali ya kwa babu ukitokea Maeda Bara. Ninasema harufu ni ya kutisha na tumekaa nayo karibu kwa mwezi mmoja na siku kadhaa. Alikuwepo mkandarasi mzuri sana ktk siku za hivi karibu aliyekuwa anaitwa KIMANGELE. Lakini sijui nini kilitokea akaletwa mtu ambaye waliona atafanya hiyo kazi, matokeo yake ni hali hii tuliyonayo sasa.

Hivi kweli tunakwenda au tunaelekea wapi? Inamaaana suala kama hili lazima liende Ikulu ndiyo lipatiwe ufumbuzi? Watu wamechukia sana. Wanauliza uongozi uko wapi? Mwenyekiti wa serikali za mtaa hapatikani kabisa maana ameshapigiwa makelele ya kutosha na nadhani kwa usalama wake amezima simu. Sijui kama kweli anapatiwa msaada mara baada ya kuwasilisha maombi au matatizo yetu. Kama tumeshindwa kuzoa hata takataka zetu tu hivi tunakoelekea ni wapi?

Moshi, Arusha na Mwanza wanafanyaje miji yao inakuwa mizuri. Tunaomba taarifa hizi ziwafikie wahusika, na tunaomba ofisi husika ziitishe mkutano na mara nyingi tunakutana pale Meeda Bar na mara hii tunaomba ulinzi wa kutosha maana wananchi wamechukia mno. Huku ni kunyanyasana kabisa. Tunaadhibiwa kwa makusudi.

Nani ambaye hajui takataka zikinyeshewa na mvua zinanuka na kutoka wadudu? Inabidi tuchemshe maji ya moto, kumwaka ili wadudu wanaotoka kwenye matakata wasiingine ndani. Mainzi ni kila kona inabidi upigie Dawa ya MBU kama Xpel au Rungu kila siku ili kuuwa wadudu. Ukisema utoe matakataka getini geti lako litapandwa kwa harufu na watu watakuona wewe ni mchafu wa kupindukia.

Wengine wamefanya hivyo baada ya matakataka kujaa getini. Hivi tunakwenda wapi na hii Sinza yetu? Hivi lazima agizo litoke kwa Waziri Mkuu ili uchafu uzolewe? Ukitaka kujua ukweli mtu yeyote kutoka serikali anayetutakia maisha mazuri, tusipate kipindupindu aje na apite katika nyumba chache tu na ajue jinsi watu walivyoumizwa na hizi takataka. Hata mtu ukiwa msafi namna gani mainzi lazima yawe sehemu ya maisha ya kila siku kwa mlundikano huu wa takataka.

Tunaomba wahusika wafuatilie hili suala la sivyo Sinza italipuka kwa kipindupindu. Hizi picha nimechukua mtaa mmoja tu yaani ni karibu nyumba kama 8 hivi. Inatisha kwa wakazi wa Sinza A. Sijui sinza B, nk. Tunaomba tusaidiwe. Na pia tunaomba kufanyike mkutano mwingine na uongozi wa mkoa ikiwezekana.

No comments: