Tuesday, March 25, 2014

Laptop ya Nguvu za Jua

Maonyesho ya wiki ya kimazingira yanayojulikana kama ‘Inhabitants Week in Green’ yanamalizika rasmi leo, lakini hayakupita bila ya kugusa hisia zetu sisi wapenzi wa gajeti, kampuni ya Fujitsu wameshusha laptop sahihi kabisa inayoendana na mazingira ya nchi kama Tanzania, hili linatokea tukiwa bado hatujasahau kwamba si muda mrefu uliopita kule Zanzibar umeme ulikatika kwa muda wa kiasi cha miezi mitatu. 

Kilichotuvutia sisi wa Gajetek katika laptop hii ambayo haikutolewa habari zake za kutosha kwa sasa ni mambo mawili. Mosi, laptop hii haihitaji chaja kabisa kwani inajichaji na paneli zenye kutumia nguvu za jua (Solar panels) zilizo kwenye eneo linalokaa kibodi na nyuma ya skrini. Pili, ni kuwa laptop hii bado imeweza kuwa nyembamba na yenye kuvutia mno kimaumbile huku ikiwa imezungukwa na paneli ya kioo (glass panel).
Hivyo umeme ukatwe mwaka mzima, wewe unaendelea na kazi zako bila ya kujali lolote kwa vile laptop hii inajichaji ikiwa inatumika na hata ikiwa haitumiki. Hivi karibuni Apple wamejigamba kuwa sasa wanaelekea kwenye hali ya ‘cable free’ wakitumia kauli ya kimatangazo (slogan) ya kata waya lakini hii ndio laptop ambayo inakupa uhuru wa kuondokana na miwaya kikweli, kwani gajeti za Apple bado zinahitaji waya ili kuzichaji.
Fujitsu hawakutoa fununu zozote juu ya ni lini laptop hii itakuwa tayari kwa mauzo au ina vianisho halisi vya aina gani. Laptop hii inatumia paneli aina ya photovoltic katika kuichaji na hivyo imeondoa mchukizo wa kisura na upana paneli za nguvu za jua za kizamani. Pamoja na uchache wa habari zake laptop hii imevutia wengi, ingawa kwa wenzetu wa nchi zilizoendelea ni suala la kimazingira tu, kwetu sisi wa nchi zinazoendelea ni suala linaloendana na hali halisi ya maisha yetu, yaani kukosa umeme kwa maeneo ya vijijini na kukatika katika kwa umeme kwa maeneo ya mijini. Tunamalizia kwa kusema hii ni laptop halisia kwa mazingira ya Tanzania.

No comments: