Tuesday, November 25, 2008

Mapenzi: Kwenye Raha Na Shida!


Picha hii niliipiga jana mchana kule Mufindi. Kuna kisa cha Bwana tajiri sana aliyefunga ndoa na mwanamke masikini. Kabla ya kufunga ndoa bwana yule aliweka sharti moja; kuwa mkewe asimwingile kwa jambo lolote. Atakachosema mume ndicho hicho hicho. Siku mke akivunja sharti hilo, basi, apewe talaka, aondoke nyumbani kwa mume akiwa amechagua moja ya mali za mume huyo. Mali ya kuondoka nayo au kuimiliki, kama ni nyumba, gari, dhahabu au shamba kubwa.

Ndani ya ndoa yao ikatokea siku moja mke yule akamkatisha mumewe katikakati ya mazungumzo. Mke alipinga hoja ya mume. Bwana yule akakasirika sana kwa mkewe kuvunja makubaliano. Akamwambia; " Unakumbuka sharti la ndoa yetu, umelivunja, fikiri sasa ni nini utachukua. Kitu kimoja kati ya mali zangu zote. Kesho asubuhi ikifika unaniambie nikupe na wende nacho kwenu.

Baada ya kauli hiyo, bwana yule kwa hasira hakutaka tena kuongea neno lolote na mkewe. Akanywa kinywaji chake kikali, akalewa na kulala kwenye sofa. Mkewe akawaomba vijana wa jirani wamsaidie kumbeba mumewe.

Alfajiri ilipofika bwana yule akajikuta ameamka nyumbani kwa wakwe zake. Akamwuliza mkewe kulikoni? Akajibiwa; E Bwana Mpendwa wangu, uliniambia nichague kitu kimoja cha kuondoka nacho kutoka nyumbani kwako, nami nimekuchagua WEWE!".

Tangu hapo bwana yule akajifunza jambo moja kubwa maishani mwake; nguvu ya pendo.

Pichani ni Berndette na Benish, raia wa Ubelgiji wanaofanya kazi Mufindi. Bernadette ameteguka mguu. OBS! Kisa nilichosimulia hakihusiani na wawili hao

No comments: